| 
| WAANDISHI wa habari wamekutana jijini Dar es Salaam na kuanza 
mchakato wa kuunda mtandao utakaoweza kusimamia, kupigania na kutetea 
haki zao. Akizungumza katika kikao hicho juzi, Katibu wa muda, Ebenezer Mende, 
alisema kuwa mtandao huo utajulikana kwa jina la ‘Waandishi wa Habari 
Tanzania (TAJONET) na utakuwa wa nchi nzima.
 Alisema mtandao huo utatumika kama chachu ya kusaidiana katika 
matatizo mbalimbali, ukiwa na sauti moja katika kutetea maslahi yao na 
utahusika moja kwa moja katika kusimamia maadili ya tasnia ya habari.
 Mende alisema kuwa hatua hiyo imekuja baada ya wandishi wa habari 
kujikuta wakikabiliwa na matatizo mbalimbali huku wakikosa msaada.
 Aidha alibainisha kuwa TAJONET utakuwa bega kwa bega katika kuangalia 
suala zima la afya ya wanachama kwa kuanzia ngazi ya chini kama matibabu
 awapo hospitalini pamoja na misiba.
 “Watu wengi wamekuwa wakichukulia matatizo ni kifo, bila kuangalia 
mambo mengine kama ugonjwa, sisi hatutaki kujielekeza hivyo bali 
tunataka tatizo la ugonjwa lipewe  kipaumbele  ili kuepusha vifo visivyo
 na ulazima,” alisema Mende.
 Alibainisha kuwa  mkutano huo umeteua viongozi wa muda  14, ambao kati
 yao wataunda kamati ya rasimu ya upatikanaji wa katiba ya mtandao huo.
 
 Chanzo: Tanzania Daima
 |  |  |