Sunday, June 17, 2012

Umeme kipaumbele Bajeti ya 2012/13 Tanzania.

 
 SERIKALI imetenga Sh498.9 bilioni katika bajeti yake ya mwaka ujao wa fedha wa 2012/13, kwa ajili ya kuongeza uzalishaji na usambazaji wa umeme nchini.
Kwa mujibu wa Waziri wa Fedha na Uchumi, Dk William Mgimwa, uzalishaji wa umeme umepewa kipaumbele kikubwa katika mafanikio ya mpango wa taifa wa maendeleo.Dk Mgimwa aliyasema hayo jana katika hotuba yake kuhusu bajeti ya Serikali katika mwaka wa fedha wa 2012/13.

Alisema katika mwaka ujao wa fedha, Serikali pia itaanza kutekeleza mradi wa ujenzi wa miundombinu ya nishati ya gesi kutoka Mtwara hadi Dar es Salaam, mradi utakaogharimu Dola 1.2 milioni za Marekani.

Kwa mujibu wa Waziri wa Fedha na Uchumi, fedha hizo zinatokana na mkopo kutoka Benki ya Exim ya China.
Dk Mgimwa alisema pamoja na umeme, miradi mingine ya maendeleo iliyopewa kipaumbele katika bajeti ya mwaka ujao, ni ya  uchukuzi, maji safi na salama.

Hali kadhalika, teknolojia ya habari na mawasiliano, kilimo, maendeleo ya viwanda na utalii.
Alisema ili kuongeza uzalishaji wa mazao ya chakula na hivyo usalama wa chakula, Serikali itahakikisha kuwa inatekeleza kikamilifu, Sera ya Kilimo Kwanza.
Alisema kiasi cha Sh192.2 bilioni kimetengwa ili kugharimia utekelezaji wa Sera ya Kilimo na kwamba fedha hizo zitatumika katika kutoa elimu kwa wakulima kuhusu kilimo cha kisasa, na kufufua kilimo cha umwagiliaji.

Pia alisema sehemu nyingine ya fedha hizo,itatumika katika kuimarisha soko la mazao kupitia Bodi ya mazao, ambayo tayari imeanza kufanya kazi.
Alibainisha kuwa kwa kushirikiana na sekta binafsi, Serikali itawekeza katika kilimo cha mpunga na miwa katika mabonde makubwa ya Wami, Ruvu, Kilombero na Malagarasi, ili kuongeza uzalishaji na thamani ya mazao.
“Pia bajeti hii imezingatia kuondoa changamoto mbalimbali zinazozua kuwepo kwa maendeleo, Serikali imedhamiria kuboresha kilimo, kuongeza ajira na kumaliza ukiritimba wa kupata mikopo kwa kuzipatia pesa taasisi  mbalimbali za fedha,” alisema waziri huyo katika hotuba yake.
Taasisi hizo ni pamoja na Benki ya Uwekezaji Nchini (TIB) iliyopewa Sh30 bilioni na Benki ya Maendeleo ya Kilimo iliyopewa Sh40 bilioni.

Dk Mgimwa alisema Serikali pia imetenga  Sh70 bilioni kwa ajili ya matumizi na maendeleo kwa mikoa na wilaya mpya.
 Eneo lingine lililopewa kipaumbele katika bajeti ya mwaka huu, ni kuimarisha miundombinu ya usafiri ikiwemo reli ya kati, usafiri wa anga na wa majini.

Kuhusu upatikanaji wa maji safi na salama, waziri Mgimwa alisema Sh568.8 bilioni zimetengwa kwa ajili ya huduma za  maji safi na salama mijini na vijijini.

Source: Mwananchi